PSG, BARCA KUIRUDISHA LEICESTER CITY DARASANI - boazmwakasege.com

MADA MOTO

Thursday, August 4, 2016

PSG, BARCA KUIRUDISHA LEICESTER CITY DARASANI


Avumaye baharini papa…….., wakati Yanga ikionekana si lolote si chochote katika mashindano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika, hapa nyumbani tunaamini Yanga ndio timu bora kwa sababu ndio bingwa wa Tanzania na pia imeonesha ubabe kwa timu nyingine za hapa nyumbani japo kwa upande wa kimataifa stori imekuwa tofauti


Nimeanza na mfano huu wa Yanga nikiifananisha na habari ya Timu ya Leicester City ya nchini England. Mabingwa hao wa Ligi Kuu ya England walikuwa moto wa kuotea mbali msimu ulioisha, wakizinyoosha timu kubwa za ligi hiyo na baadaye kuibuka mabingwa.

LEICESTER CITY (1)

Leicester ndio mabingwa wa Ligi Kuu England na wataiwakilisha nchi katika mashindano makubwa ya Uefa Champions League ikiwa ni mara yao ya kwanza tangu kuanzishwa kwake. Katika mashindano hayo makubwa Leicester itakwaana na vigogo wa soka barani Ulaya ambapo ili kufika mbali lazima wajifue kisawasawa.

Taswira ilishaanza kujionyesha hasa katika mashindano ya International Champions Cup yanayoendelea, Leicester City ilipokea kipigo cha mabao 4-0 toka kwa mabingwa wa Ufaransa, Paris Saint-Germain wiki iliyopita na jana ikikubali kichapo tena cha mabao 4-2 toka kwa mabingwa wa Spain Barcelona. Hii inaashiria nini?

Katika michuano ya Uefa Champions League hakuna legelege, lazima timu husika ijitathmini vilivyo, ukizingatia kule unakutana na vigogo ambao wana vikosi bora, vilevile wana uzoefu mkubwa katika michuano hii. Timu kama Bayern Munichen, Juventus, Real Madrid, Barcelona na nyinginezo huwezi kuzikwepa kukutana nazo, iwapo unakubali kunyanyaswa na baadhi ya timu hizi unatarajia nini katika mashindano?

LEICESTER CITY (2)

Naiona Leicester City ambayo haitaweza kutoa ushindani mkubwa katika mashindano ya UCL, naamini watapambana kwa nguvu zao zote lakini kuna baadhi ya vigezo wanakosa. Kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu England pekee haitoshi kukufanya mbabe katika bara la Ulaya, hata Manchester City wana kikosi bora sana katika miaka ya karibuni lakini hawajaweza kuonyesha maajabu zaidi katika mashindano ya UCL.

Vipigo ilivyopokea Leicester City toka kwa PSG na BARCA ni fundisho tosha kwa timu hii kujitathmini na kujitazama kabla ya kuanza kutupa karata yake ya kwanza kwenye mashindano.

No comments:

Post a Comment