BAKWATA –acheni tabia ya kuhusisha Dini ya Kiislamu na matukio ya Kigaidi. - boazmwakasege.com

MADA MOTO

Monday, December 12, 2016

BAKWATA –acheni tabia ya kuhusisha Dini ya Kiislamu na matukio ya Kigaidi.


BARAZA Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) limesikitishwa na tabia iliyoanza kujengeka ya kuihusisha Dini ya Kiislamu na vitendo vinavyoashira ugaidi vilivyojitokeza nchini katika siku za hivi karibuni na kugharimu maisha ya watu.

Kwa hiyo, limependekeza kuundwa kwa kamati maalumu ya kitaifa na mkoa kwa ajili ya kuangalia suala hilo kwa undani zaidi ili kuondoa hofu inayojengeka katika jamii dhidi ya Uislamu.

MUFTII_800_600 

Wito huo ulitolewa jana na katibu mkuu wa Bakwata, Sheikh Suleiman Lolila wakati akitoa salamu kwenye Baraza la Maulid lililofanyika kitaifa wilayani Iramba, mkoani Singida.

Alisema miezi kadhaa iliyopita pamekuwepo na matukio ya kutisha maeneo ya Mwanza, Mkuranga mkoani Pwani, Morogoro na Tanga ambayo yamesababisha vifo vya Watanzania kadhaa wasio na hatia.

“Baraza Kuu la Waislamu Tanzania limesikitishwa sana na matukio hayo ambayo yameleta vifo vingi. Baraza linasikitika sana Uislamu kuhusishwa na ugaidi,” alisema Lolila.

Alibainisha kuwa suala linalowasikitisha zaidi Waislamu ni wahalifu hao wa ugaidi mara nyingi kujitambulisha kuwa ni waumini wa dini ya Kiislamu.

Alisisitiza kuwa Uislamu hauungi mkono vitendo hivyo vya ugaidi kwa kuwa ugaidi ni haramu, hivyo ni lazima upigwe vita kwa namna yoyote ile.

Alisema Mtume Muhammad   alihimiza amani, umoja na mshikamano baina ya Waislamu wote ambapo alilinganisha umoja huo sawa na viungo vya mwanadamu.

Aidha, Bakwata itaendelea kukariri wito wake wa kuwataka Waislamu nchini kuondoa mafarakano baina yao na kuimarisha umoja, mshikamano na mambo yote yenye maslahi kwao.

 Chanzo: MTEMBEZI.COM

No comments:

Post a Comment